Kwa mujibu wa Shirika la Habari la Kimataifa la Ahlul-Bayt (as) –ABNA– Mamilioni ya waumini walioshiriki katika mazishi ya Kiongozi Shahidi wa Mapinduzi ya Kiislamu, Ayatollah Mkuu Sayyid Ali Husseini Khamenei, waliinua mikono yao kwa dua katika Sala ya Maiti, wakimshuhudia mbele ya Mwenyezi Mungu kuwa alikuwa mja mwema aliyelitumikia kwa uaminifu dini na Umma wa Kiislamu.

Sala ya Maiti ni miongoni mwa ibada muhimu katika hukumu za Kiislamu zinazohusiana na maandalizi ya mazishi ya Muislamu. Baada ya kuoshwa na kuvishwa sanda, waumini husimama kuelekea Qibla huku mwili wa marehemu ukiwa mbele yao, kisha huswali Sala ya Maiti ambayo inajumuisha dua za kumuombea marehemu rehema, msamaha na kuinuliwa daraja zake mbele ya Mwenyezi Mungu.

Katika fiqhi ya Shia, kiwango cha lazima cha Sala ya Maiti ni kifupi, lakini inapendekezwa kuongeza dua nyingi za kumuombea marehemu kila aina ya kheri na rehema za Mwenyezi Mungu.

Aidha, idadi kubwa ya watu wanaoshiriki katika Sala ya Maiti imekuwa ikionekana katika jamii za Kiislamu kuwa ni ishara ya mapenzi, heshima na nafasi ya marehemu katika nyoyo za waumini. Hivyo, mamilioni ya walioshiriki katika mazishi ya Kiongozi Shahidi walidhihirisha kwa vitendo mapenzi yao, huku wakimuombea Mwenyezi Mungu amjaalie daraja ya juu na amfunike kwa rehema Zake pana.



Your Comment